Jaji Warioba afurahishwa na mafunzo yanayotolewa kusaidia vijana nchini

Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA Jaji Mstaafu Mhe. Joseph Sinde Warioba amefurahishwa na mafunzo yanayotolewa SUA kwa kushirikiana na PASS (Private Agricultural Support Sector) yanayosaidia  vijana kujiajiri na jamii kwa ujumla.

SUA

Mhe. Jaji Warioba ametoa pongezi hizo leo octoba 25, 2021 katika ziara yake ya siku mbili hapa Chuoni, akiwa ameambatana na Mwenyekiti wa baraza la Chuo Jaji Othman Chande na makamu mwenyekiti wake Bi. Doroth Mwanyika.

“Hawa vijana wakitoka hapa watasaidia kuwa walimu kwa jamii inayowazunguka na tayari wana kitu cha kufanya ukweli nimefurahi sana kuona vijana kutoka Mikoa mbalimbali kama Tabora, Mwanza, Kigoma, Rukwa wakipata mafunzo haya” alisema Mhe. Jaji Warioba.

Aliongeza “mafunzo hayo yatasaidia Taifa letu kwa kiasi kikubwa hususani miaka ijayo katika kukidhi mahitaji ya chakula na kuepukana na balaa la njaa kutokana na ongezeko la watu kwani wakati nchi inapata uhuru tulikuwa Watanzania milioni 9 lakini sasa wamefika milioni 60 hivyo tutarajie ongezeko kubwa la watu na uhitaji mkubwa Chakula”. 

Pia amewataka SUA kuongeza elimu kwa upana ili kuwafikia vijana wengi zaidi kwani mafunzo hayo tayari yameshaleta mafanikio kwa jamii kupitia vijana waliopita ambao waliopata mafunzo hayo.
Kwa upande wa Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA Prof. Raphael Chibunda amemshukuru  Mkuu huyo wa Chuo kwa kazi kubwa aliyoifanya katika kipindi cha miaka minne na mafanikio yaliyopatikana.

Profesa Chibunda amesema kuwa wamefanya maboresho makubwa Chuoni hapo kwa kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia  kwa wanafunzi hususani mashamba ya kujifunzia kwa vitendo ili kujifunza kwa vitendo ikiwemo ujenzi wa maabara ikiwemo maabara mtambuka ambayo inweza kuchukua wanafunzi 3200  kwa wakati mmoja pamoja na ununuzi wa vifaa vya kisasa vya maabara hizo.

Makamu Mkuu wa Chuo pia amesema kuwa Chuo kimetenga fedha zaidi ya milioni 450 kwaajili ya kujenga vitalu 100 katika kipindi cha miaka mitatu, ambapo kwa mwaka huu wataanza na vitalu 30 na tayari wamepeleka maombi mahususi kwa Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) kwa lengo la kushirikiana kuendeleza wabunifu kwa kujenga vitalu vingi zaidi.

Aidha, ameongeza kuwa tayari milioni 200 imetumika kwaajili ya upanuzi wa sehemu ya upasuaji kwenye Hospitali ya rufaa ya Wanyama SUA na manunuzi ya vifaa vipya kama mashine ya X- Ray Digital,Ultra Sound  ya kisasa yenye kuwezesha kuona kama mnyama amepata tatizo kubwa zaidi kwa ndani lakini  pia Chuo kipo mbioni kununua gari litakayotumika kama kliniki inayotembea ili kuwafikia wafugaji wanaoshindwa kufika kwenye hospital hiyo ya Taifa ya rufaa ya wanyama ili kupatiwa matibabu. 

“Nitoe wito kwa wafugaji wa Wanyama katika nchi hii pale wanapoona wamekosa msaada sehemu nyingine basi waitazame Hospitali yetu ya Rufaa ya Taifa ya Wanyama kama sehemu ya kupata msaada” amesema Profesa Chibunda.

Katika ziara hiyo Jaji Mstaafu Mhe. Joseph Sinde Warioba ametembelea Ndaki mbalimbali ikiwemo Ndaki ya Tiba ya wanyama na sayansi za afya, Ndaki ya Kilimo kwenye Shamba la mafunzo, Maabara mtambuka,Kituo atamizi cha Vijana kilichopo chini ya Shule kuu ya uchumi kilimo na taaluma za biashara, kitengo cha mifugo Magadu, kitengo cha Samaki magadu na maabara ya sayansi na teknolojia ya chakula.

Story and Photo Credits
Calvin Gwabara - SUAMEDIA

Share this page